Latest Updates

Wosia wa Mandela watangazwa




Johannesburg. Wosia wa aliyekuwa Rais wa Kwanza mzalendo wa Afrika Kusini, Nelson Mandela umesomwa huku mgawanyo wa mali zake ukielekezwa katika maeneo tofauti.
Katika wosia huo uliosomwa rasmi jana, Mandela aliacha mali zenye thamani ya Dola za Marekani 4.1 milioni, sawa na Sh5.6 bilioni ambazo zimepangwa kugawiwa kwa taasisi mbalimbali, familia na wafanyakazi wake.
Katika wosia huo ulioandikwa na Mandela mwenyewe mwaka 2004 na kufanyiwa marekebisho mwaka 2008, mkewe, Graca Machel anapata karibu nusu ya mali zake zote alizoziacha.
Mali hizo zinajumuisha nyumba kubwa alizokuwa akimiliki moja ikiwa Johanesburg, nyingine Qunu na ya tatu Mthatha. Mali nyingine ni sehemu ya mrabaha aliyokusanya baada ya kuuza machapisho mbalimbali ikiwamo kitabu chake maarufu cha “Long Walk to Freedom” ambacho kinatajwa kuuzwa kwa wingi duniani.
Pia sehemu za mali hizo zimetokana na kazi mbalimbali alizozifanya wakati akiwa rais na baada ya kuachia madaraka na kujihusisha na wakfu wake wa Mandela Foundation. Wakfu huo ndiyo uliofanikisha kuratibu shughuli mbalimbali za kijamii ambazo alizitekeleza baada ya kustaafu.
Kutangazwa kwa mali hizo kumemaliza minong’ono ya muda mrefu iliyokuwa ikihusisha sehemu kubwa ya familia yake ambayo imewahi kuingia kwenye malumbano juu ya nani anayepaswa kumiliki mali hizo.
Akisoma wosia ulioachwa na Mandela mbele ya waandishi wa habari, Naibu Jaji Mkuu Dikgang Moseneke alisema wanafamilia ya Mandela wamekubaliana na yote yaliyoandikwa na hakuna pingamizi lolote lililotijokeza.
Hata hivyo, kuna nafasi ya kuweka pingamizi juu ya wosia huo katika kipindi cha siku 90 kuanzia sasa vinginevyo, baada ya hapo utaanza kutekelezwa mara moja.
Wosia huo uliokuwa na kurasa 40 umeorodhesha watu na taasisi zinazostahili kuwa sehemu ya mgawanyo huo wa mali na kutaja kiwango stahili kinachopaswa kutolewa.
Chama cha ANC ambacho Mandela na marafiki zake walikiasisi kwa ajili ya kukabiliana na siasa za kibaguzi wakati wa utawala wa makaburu ni miongoni mwa taasisi ambazo zitapitiwa na mgawo huo.
Kamati Kuu ya ANC inatazamia kutumia fedha hizo kwa ajili ya kusambaza sera na misingi ya chama inayohusu maridhiano.
Wengine waliotajwa kwenye urithi huo ni pamoja na aliyekuwa msaidizi wake katika siku zake za mwisho, Zelda la Grange, Chuo Kikuu cha Wits, Shule ya Sekondari ya Qunu na Shule ya Sekondari ya Orlando iliyoko Soweto.
                                       Dj Sek 

0 Response to "Wosia wa Mandela watangazwa"

Post a Comment